Kijiji cha Mwabayanda ni miongoni mwa vijiji vinavyounda Kata ya Ng’wigwa ambapo kwa muda mrefu hakikuwa na huduma ya afya hivyo kupelekea wananchi wake kutembea umbali mrefu wa kilometa 15 kwenda kijiji cha Igongwa au Hospitali ya Wilaya ya Maswa kupata huduma.
Serikali ya kijiji hicho cha Mwabayanda kwa kushirikiana na wananchi walijenga boma la Zahanati hiyo ambapo serikali ya Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan katika kuunga mkono jitihada za wanachi hao ilitoa shilingi milioni hamsini kwa ajili ya ukamilishaji wa zahanati hiyo.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo mgeni rasmi Ndg. Marko Nkwimba ambaye alimwakilisha Mkuu wa Wilaya ameishukuru Serikali ya awamu ya sita kwa kupeleka fedha katika kijiji hicho ambayo imesaidia wananchi hao kuanza kupata huduma mbalimbali za kiafya katika zahanati hiyo.
Pia Ndg Nkwimba aliwashukuru wananchi kwa ushirikiano waliouonesha kwa kujitolea nguvu kazi mpaka Zahanati hiyo ikakamilika. Pia aliwataka waache tabia zisizo nzuri za mila potofu ambazo zitasababisha mtumishi huyo kushindwa kukaa hapo.
Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Wilaya ya Maswa Dkt Adorat Mpollo alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kutoa shilingi milioni mia mbili kwa ajili ya kukamilisha maboma manne ikiwemo zahanati ya Mwabayanda “M” ambayo ilipata shilingi milioni hamsini kwa ajili ya kukamilisha zahanati hiyo pamoja na shilingi milioni hamsini na tano kwa ajili ya nyumba ya mtumishi ambazo zilitoka katika mfuko wa TASAF.
Aidha alimshukuru Mhe. Diwani wa Kata ya Ng’wigwa kwa usimamizi mzuri wa miradi inayotekelezwa katika Kata yake pamoja na Mwenyekiti wa Kijiji na timu yake kwa kusimamia vizuri mradi wa zahanati hiyo mpaka ikakamilika na kuanza kutoa huduma za kimatibabu.
“Tunawashukuru wananchi kwa ushirikiano wao wote ambao wameuonyesha kwa Halmashauri ya Wilaya ya Maswa kwa kutoa nguvu zao hili jengo mpaka lilipofikia kwa nguvu za wananchi sio jambo la kitoto, lakini pia kutoa nguvu zao katika ujenzi wa nyumba ya mtumishi”.
Mganga Mkuu wa Wilaya alitoa wito kwa akina mama wajawazito na watoto kuwahi katika zahanati kwa kuwa huduma imesogezwa karibu ili kuepukana na vifo vinavyotokana na uzazi pia ametoa rai kwa akina mama kuacha tabia za kujifungulia nyumbani au kwa wataalamu wa mitaani.
Dkt mpollo alieleza kuwa serikali inaendelea kuboresha sekta ya afya ambapo mwaka wa fedha wa 2023/2024 Hospitali ya Wilaya imewekewa bajeti ya shilingi milioni mia tisa kwa ajili ya ukarabati wa majengo katika Hospitali hiyo.
Kwa upande wao wanachi wameishukuru serikali kwa kuwasogezea huduma hiyo katika kijiji hicho na wameahidi ushirikiano kwa mtumishi wa zahanati hiyo na kuomba serikali iwaongezee watumishi wengine kwa kuwa wananchi ni wengi watakaoenda kupata huduma hapo.
Halmashauri ya Wilaya ya Maswa
Sanduku la Posta: 170, MASWA
simu ya Mkononi: +255 282 750 271
Simu: +255 282 750 271
Barua Pepe: ded@maswadc.go.tz
Copyright ©2022 Maswa District Council. All rights reserved.