Mkuu wa Wilaya ya Maswa Mhe Aswege Kaminyoge amesema Serikali ya awamu ya sita imetenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa Barabara mbalimbali katika mji wa Maswa ambao utabadili muonekano wa mji na kukuza uchumi na biashara katika wilaya ya Maswa.
Akitoa salamu za Serikali leo tarehe 8 Septemba 2022 katika Baraza la madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Maswa lililofanyika katika ukumbi wa Halmashauri hiyo, Kaminyoge amesema tayari Serikali imetoa Shs. bilioni 11 kwa ajili ya ujenzi wa Barabara ya Mchepuo (buypass) ambapo maroli yatapita huko na kuepusha msongamano na ajali katika maeneo ya mjini.
Aidha Mkuu wa Wilaya amewaomba Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Maswa, Mwenyekiti wa Halmashauri, waheshimiwa madiwani pamoja na wataalamu wote kutengeneza alama yenye muonekano mzuri ambayo itautambulisha mji wa Maswa kutokana na ujenzi wa barabara ya mzunguko (roundabout) itakayojengwa Njiapanda ya Lalago na Lalago Maswa Girls.
Pia Mhe Kaminyoge amewapongeza Waheshimiwa Madiwani kwa kusimamia vizuri zoezi la Sensa ya watu na makazi kwa kuwa hakuna kaya hata moja ambayo haijahesabiwa na zoezi la chanjo ya porio ambapo Wilaya ya Maswa imevuka lengo katika zoezi hilo.
Awali wakiwasilisha taarifa kwa nyakati tofauti za utekelezaji wa miradi ya maji na Barabara wakala wa Barabara za vijijini na mjini (TARURA) na Mamlaka ya maji na Usafi wa Mazingira Mjini Maswa (MAUWASA) wamesema Serikali itaendelea kutoa fedha ili miradi yote ambayo haijakamilika ikamilike na wananchi wapate huduma Bora ambazo zitawawezesha kufanya maendeleo katika maeneo yao.
Kwa upande wao waheshimiwa Madiwani wameipongeza serikali kwa jitihada kubwa walizozifanya kwa kutumia fedha za tozo katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya barabara na maji na kuomba serikali iendelee kutoa fedha ili Miradi ambayo haijakamilika iweze kukamilika.
Halmashauri ya Wilaya ya Maswa
Sanduku la Posta: 170, MASWA
simu ya Mkononi: +255 282 750 271
Simu: +255 282 750 271
Barua Pepe: ded@maswadc.go.tz
Copyright ©2022 Maswa District Council. All rights reserved.