Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Dkt Yahaya Nawanda ametoa kongole kwa viongozi wa Wilaya ya Maswa kwa kusimamia vizuri ujenzi wa miradi ya elimu inayoketelezwa katika maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Maswa.
Mkuu wa Mkoa alisema hayo kwa nyakati tofauti wakati akikagua miradi ya ujenzi wa shule mpya 2 za Sekondari zilizopo Kata ya dakama na kulimi ambapo ujenzi huo umegharamiwa na serikali kupitia mradi wa kuimarisha Elimu ya sekondari (SEQUIP ) ambapo kila shule ilipata kiasi cha shilingi milioni 584,200,000/= na ujenzi upo katika hatua ya ukamilishaji.
Aidha Mhe Dkt Nawanda alitembelea ujenzi wa shule mpya ya msingi Jija A yenye mikondo miwili na kuwapongeza Wilaya ya Maswa kwa kuweka fensi katika shule ya awali ili kuwalinda watoto wa chekechea ambao watasoma hapo ambapo, pia alikagua ukarabati wa shule ya msingi Malampaka.
Aidha alitembelea ujenzi wa jengo jipya la Utawala ambalo linajengwa katika Kitongoji cha Ng'hami Kata ya Nyalikungu ambapo mradi huo upo katika hatua ya msingi ambapo serikali imetoa kiasi cha shilingi bilioni 1 kwa ajili ya ujenzi huo awamu ya kwanza (Phase one) sambamba na ujenzi wa nyumba ya mtumishi ya 2 in 1 katika shule ya sekondari Mashimba serikali kuu ilitoa kiasi cha shilingi milioni 100 ambapo ujenzi upo katika hatua ya ukamilishaji.
Mkuu wa Mkoa alimshukuru Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kutoa Fedha nyingi ambazo zimewezesha wananchi wa maeneo hayo kupata miundombinu ya Elimu ambayo itawasaidia watoto hao kusoma katika Mazingira mazuri.
Dkt Nawanda amewashukuru wananchi wa Maswa kwa utoaji wa chakula mashuleni ambapo katika Mkoa wa Simiyu Wilaya ya Maswa inaongoza kwa utoaji wa chakula shuleni kutokana na sifa hizo amewataka waendelee kuchangia chakula ili watoto wao wasome vizuri na kufaulu mitihani yao kwa wastani unaotakiwa.
Katika hatua nyingine Mhe. Dkt Nawanda amewataka wananchi kuchukua tahadhari mapema pindi mvua za El-nino zitakapoanza kwa kuhama maeneo ambayo yatakuwa hatarishi na amesisitiza wananchi kutokuuza chakula chote katika kipindi hicho
Ametoa wito kwa viongozi wote kuanzia ngazi ya Wilaya mpaka Kata kuandaa mpango wa kutenga maeneo ya kuwahifadhi wananchi pindi mvua zitakapozidi na kusababisha maeneo yao kuwa na maji mengi.
Akiwa Wilayani Maswa Mkuu wa Mkoa amezungumza na wanachi katika maeneo tofauti alipokuwa akikagua miradi hiyo na kutatua kero mbalimbali zilizokuwa zinawakabili wananchi wa maeneo hayo sambamba na hilo amewataka wananchi kuchangamkia fursa kwa kuchukua mbegu za pamba ambazo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan ametoa bure kwa ajili ya wakulima wote kulima kwa wingi zao hilo.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Maswa Mhe. Aswege Kaminyoge amempongeza Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kutoa Fedha nyingi kwa ajili ya kujenga miundombinu mbalimbali ya maji, umeme, barabara, Elimu na afya ambapo wananchi wa Maswa wanapata huduma hizo vizuri.
Halmashauri ya Wilaya ya Maswa
Sanduku la Posta: 170, MASWA
simu ya Mkononi: +255 282 750 271
Simu: +255 282 750 271
Barua Pepe: ded@maswadc.go.tz
Copyright ©2022 Maswa District Council. All rights reserved.