Afisa lishe wa Wilaya ya Maswa Ndg Abel Gyunda amewataka vijana wa rika balehe kutumia mlo kamili unaohusisha makundi matano ya chakula lengo likiwa ni kumsaidia mwanafunzi kuwa na uwezo mkubwa wa kuelewa darasani pamoja na kukua vizuri kimwili, kiafya na kisaikolojia ili kuepukana na udumavu, uzito kupita kiasi pamoja na ukondefu.
Ndg Gyunda ameyasema hayo katika maazimisho ya siku ya lishe duniani ambayo kiwilaya yamefanyika katika shule ya sekondari ya wasichana Maswa leo tarehe 30/10/2023 wakati akitoa Elimu ya namna bora ya kula mlo kamili kwa wanafunzi wa lika la vijana balehe ambapo wanafunzi pamoja na walimu walishiriki katika maadhimisho hayo.
Lengo la maadhimisho hayo ni kujenga uelewa kwa jamii juu ya umuhimu wa lishe bora kwa vijana balehe na kuhamasisha sekta mbalimbali kuweka kipaumbele katika masuala ya lishe hasahasa kwa vijana kuanzia miaka 10-19.
Aidha amesema katika rika la vijana balehe ongezeko la virutubishi mwilini huongezeka kutokana na viungo vyao kukua hivyo ametoa ushauri kwa kundi hilo kutumia lishe bora ili kukabiliana na mabadiliko hayo.
Afisa lishe ametoa wito kwa vijana balehe kuepuka kula vyakula vyenye sukari nyingi, matumizi ya vileo, chumvi nyingi, na mafuta mengi kwa sababu ni hatarishi kwa lishe katika rika hilo hivyo vijana hao wanatakiwa kupata kirutubishi cha madini chuma ambayo ni muhimu sana katika kuongeza wingi wa damu mwilini.
Ameongeza kuwa vijana hao wanatakiwa kujishughulisha kwa kufanya kazi na sio kukaa tu bila kazi lengo likiwa ni kupunguza lishe duni katika kundi hilo ambalo kwa kiasi kikubwa linapata athari ya kupungua kwa nguvu kazi kwa kutokufanya maamuzi ya busara pamoja na udumavu kutokana na viungo kutokuwa sawasawa ambapo husababisha magonjwa sugu yasiyo ya kuambukizwa ambayo ni kisukari, saratani na shinikizo la damu.
Maadhimisho hayo yameenda sambamba na tahmini ya hali ya lishe kwa kupima urefu pamoja na uzito kwa kundi hilo la rika la vijana balehe ambapo tahmini imeonyesha kundi hilo linazingatia lishe bora na pia amewaomba waendelee kutumia vyakula hivyo kwa wingi ili kuepukana na udumavu.
Halmashauri ya Wilaya ya Maswa
Sanduku la Posta: 170, MASWA
simu ya Mkononi: +255 282 750 271
Simu: +255 282 750 271
Barua Pepe: ded@maswadc.go.tz
Copyright ©2022 Maswa District Council. All rights reserved.