Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Maswa Ndg. Maisha Mtipa amewataka wananchi wa Maswa kulima Kilimo bora kwa kutumia mbegu bora ambazo zimefanyiwa utafiti kwa kuwa Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ametoa Fedha nyingi kwa ajili ya kuboresha sekta ya Kilimo ili wananchi waweze kuongeza tija na kuzalisha kwa tija.
Ndg Mtipa aliyasema hayo katika kilele cha maonesho ya sikukuu ya nanenane Kanda ya Ziwa Mashariki yaliyofanyika katika uwanja wa Nyakabindi, Bariadi mkoani Simiyu wakati akitembelea vipando vya mazao mbalimbali vya Halmashauri ya Wilaya ya Maswa na kuona namna ambavyo mbinu Bora za Kilimo zilivyotumika.
Aidha Mkurugenzi Mtendaji alisema mazao yote yakilimwa kwa kufuata utaalamu yatawasaidia kuongeza tija na ametoa wito kwa vijana na wanawake kushiriki kikamilifu katika Kilimo ili waweze kuleta mifumo endelevu ya chakula.
Kwa upande wake Mkuu wa Divisheni ya Kilimo Mifugo na Uvuvi Ndg. Robert Urassa wa Halmashauri ya Wilaya ya Maswa amewataka wananchi na taasisi za umma hasahasa shule kulima zao la alizeti ili liwawezeshe kupata huduma ya mafuta kwa ajili ya kupikia.
“Mikakati ya wilaya ya Maswa ni kuhakikisha zao la alizeti linapandwa na tayari lilianza msimu wa mwaka juzi tulihamasisha wananchi vizuri, kuwaletea mbegu pia tunaendelea kuhamasisha wananchi wapande zao la alizeti, Alizeti ni zao litakalomkomboa mkulima”. Amesema Ndg Urassa.
Nae Bw. Masuka Balele ambaye ni bwana shamba katika kampuni hiyo ya usambazaji wa mbegu mbalimbali kutoka katika kampuni ya Advanta amewaomba wananchi wa Maswa kuchangamkia fursa ya mbegu za alizeti aina ya chotara katika msimu ujao wa Kilimo zenye mafuta mengi, zinazohimili magonjwa, wadudu na kupata mavuno mengi yenye ujazo wa kuanzia gunia 15 mpaka 16 kwa hekari.
Nae mkulima wa mbogamboga Ndg Simon William amewataka wananchi wa Maswa wawe wanahudhuria katika maonesho ya nanenane ili waweze kupata utaalamu wa mbinu Bora za Kilimo kwa kuwa yeye kimemsaidia kujiinua kiuchumi na kupata lishe Bora katika familia yake.
Halmashauri ya Wilaya ya Maswa
Sanduku la Posta: 170, MASWA
simu ya Mkononi: +255 282 750 271
Simu: +255 282 750 271
Barua Pepe: ded@maswadc.go.tz
Copyright ©2022 Maswa District Council. All rights reserved.