Mkuu wa wilaya ya maswa Mh. Aswege Kaminyoge amezindua rasmi operesheni ya uwekaji wa anwani za makazi na postikode itakayotekelezwa wilayani Maswa.
Operesheni hiyo imezinduliwa leo March 15 katika eneo la Madeko na kuhudhiriwa na viongozi mbalimbali wa wilaya wakiwemo Kamati ya ulinzi na usalama wilaya, Kamati ya anwani za makazi, wataalamu wengine wa halmashauri, Vijana watakao husika katika zoezi la ukusanyaji taarifa za anuani za makazi pamoja na wananchi.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kuweka kibao cha anwani katika Barabara ya Uhuru na Kadoto iliyopo hapa Maswa Mkuu huyo wa Wilaya amesema Barabara hizo ndizo zitakazotumika katika utambuzi wa anwani za makazi (postikode) na zoezi hilo litaendelea maeneo yote ya Wilaya ya Maswa.
Mh. Kaminyoge ameongeza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Samia Suluhu Hassani ametoa maelekezo hayo kwa nchi nzima kuwa maeneo yote lazima yatambulike kwa sababu ni sera ya taifa ya mwaka 2003 ya posta kuwa ifikapo 2025 kila nyumba, taasisi, biashara, hospitali na maeneo mengine yote na barabara yawe na namba zinazoeleweka
Aidha Mkuu wa Wilaya amewaeleza wananchi lengo la kuweka anwani za makazi litawaletea manufaa makubwa katika shughuli mbalimbali wanazozifanya ikiwepo biashara mtandaoni, kurahisisha shughuli za tafiti na upatikanaji wa taarifa, kuimalisha ulinzi na usalama pamoja na upatikanaji wa huduma kwa urahisi katika maeneo husika.
Mh. Kaminyoge ametoa wito kwa viongozi wote kuanzia ngazi ya Kitongoji, Vijiji, Kata na Ofisi ya Mkurugenzi waendelee kutoa elimu ili kurahisisha zoezi hilo na kuwapa ushirikiano na mazingira wezeshi vijana wote waliopata mafunzo ili waweze kufanya kazi kwa ubunifu na weredi mkubwa kwa sababu zoezi hilo linatakiwa kukamilika ifikapo April 15.
Halmashauri ya Wilaya ya Maswa
Sanduku la Posta: 170, MASWA
simu ya Mkononi: +255 282 750 271
Simu: +255 282 750 271
Barua Pepe: ded@maswadc.go.tz
Copyright ©2022 Maswa District Council. All rights reserved.