Mkuu wa Wilaya ya Maswa Mhe. Aswege Kaminyoge ameagiza wakulima wote waliolima pamba wanatakiwa kupewa mabomba kwa ajili ya kunyunyizia sumu katika mashamba yao ya pamba kuepukana na wadudu kuharibu mazao.
Mhe Kaminyoge amezungumza hayo katika baraza la madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Maswa katika kikao cha robo ya pili mwaka wa fedha 2022/2023 katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Maswa wakati akitoa salamu za serikali.
Mkuu wa Wilaya amesema kuwa mwaka huu AMCOS imenunua pamba kutoka kwa wananchi ambapo kupitia fedha hizo Halmashauri ya Wilaya ya Maswa imenunua bomba ambazo zimegawiwa katika vijiji 120 kwa ajili ya kuwagawia wakulima pamoja na bodi ya pamba Tanzania ambayo imetoa bomba za kunyunyizia sumu na viuatilifu.
Mhe. Kaminyoge ameipongeza serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe. Dkt Samia Suluhu Hasan kwa kutoa viuatilifu bure ambavyo ni vizuri kwa kuwa vinaua wadudu na vina ubora.
Ameongeza kuwa wakulima wote waliolima heka kuanzia 10 na kuendelea wenye uwezo wa kuuza mifugo yao kama vile mbuzi wanunue mabomba yao wenyewe kwa ajili ya kupulizia mashamba yao ya pamba kuliko kusubiri bomba la kuazima kwa sababu mkulima akimiliki bomba lake mwenyewe litamsaidia mkulima kunusuru pamba yake na kupata mavuno mazuri.
Amesisitiza kwa kumwagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Maswa kutoa waraka / mwongozo ambao utamfanya kila mkulima aliyelima pamba aweze kupata bomba hizo kupitia watendaji wa vijijini ambao watashirikiana na kamati za vijiji kujua idadi kwa ajili ya kukabidhi kwa wenyeviti wa vitongoji ili waweze kuwapa wananchi wao kutumia katika kupulizia mashamba yao.
Pia Mhe. Mkuu wa Wilaya ametoa onyo kwa wananchi au maduka binafsi yanayouza viuatilifu kuwa yeyote atakayekutwa anauza viuatilifu hivyo madukani na mnadani hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yake na hakutakuwa na dhamana kwake kwa kuwa atahesabika kama mhujumu uchumi.
Aidha, Mhe. Kaminyoge amewasisitiza waheshimiwa madiwani kufanya mikutano kwa kuwa serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe. Dkt Samia Suluhu Hasan imejitangaza yenyewe kwa kutekeleza miradi Mikubwa ya kati na midogo hivyo ni jukumu la viongozi kuwaeleza wananchi jinsi serikali ilivyofanya na inavyoendelea kufanya kazi.
Halmashauri ya Wilaya ya Maswa
Sanduku la Posta: 170, MASWA
simu ya Mkononi: +255 282 750 271
Simu: +255 282 750 271
Barua Pepe: ded@maswadc.go.tz
Copyright ©2022 Maswa District Council. All rights reserved.